05/06/2022
Historia ya umangi Rombo,maeneo ya usseri..
Mangi Matolo ni kati ya Wamangi wa Usseri waliokuwa maarufu sana katika historia.
Mangi Matolo na Mangi Malamia wote walikuwa ni watoto wa Mangi Kafuria wa Usseri.
Mangi Kafuria ndiye alipambana na majeshi ya Mangi Horombo akashindwa lakini baadaye ndiye aliyekuwa chanzo cha anguko la Mangi Horombo.
Baada ya Mangi Kafuria kufariki kiti cha umangi wa Usseri kilikaliwa na mtoto wake Malamia.
Mangi Malamia alitawala Usseri kwa muda mrefu na alikuwa imara pia lakini alipofariki mtoto wake aliyeitwa Kisuma alichukua madaraka lakini inasemekana hakukaa muda mrefu alipinduliwa na ndugu yake Malamia aliyeitwa Matolo.
Mangi Matolo ambaye ni ndugu yake Mangi Malamia aliitawala Usseri baada ya hapo kwa muda mrefu sana na kisha baada yake akarithisha kiti cha utawala kwa mtoto wake aliyeitwa Salakana.
Baada ya Salakana akaingia ndugu yake mwingine aliyeitwa Ndemasi kisha mtoto wa Salakana tena.
Hata hivyo inasemekana kuna mtoto wa Mangi Malamia aliyeitwa Nambua ambaye alikuja kufanywa kuwa Mangi wa Ngasseni baadaye wakati wa utawala wa Wajerumani.